‘RAIS’ WA JANG’OMBE BOYS AAHIDI KURUDIA TENA KUWALIZA KMKM KATIKA LIGI KUU YA ZANZIBAR



Hatimae pazia la ligi kuu Zanzibar kufunguliwa hapo kesho tarehe 03 Oktoba, ambapo mapema saa nane za mchana kutakuwa na mchezo kati ya maafande wa vikosi vya JKU na Mafunzo na Jang’ombe Boys FC tutachuana na KMKM saa 10.00 alasiri.

Na: Mwandishi wetu.

Katika mchezo huo kati yetu na KMKM mshambuliaji wetu machachari kwa kuzifumania nyavu za timu pinzani, Khamis Mussa Makame (Rais), ameendelea kutoa vitisho kwa vilabu vinavyoshiriki ligi hio kwa kuwa anaamini kwa sasa ameimarika zaidi hivyo yuko tayari kwa mchezo na timu yeyote wakati wowote, na kuzidisha kwamba timu yeyote itakayoingia uwanjani ikiwa mwalimu atampanga basi wategemee kupokea kichapo kutoka kwake.

Mshambuliaji mahiri wa Jang'ombe Boys
Khamis Mussa 'Rais'


“Mimi binafsi yangu niko tayari kwa mchezo wa kesho na michezo yote ya ligi kuu, kama nilivyowaliza KMKM msimu uliopita kwa goli langu moja na jengine kufungwa na mwenzangu ‘Chinga’, basi niseme kesho 'Insha Allah' nitaweka nyavuni zaidi ya goli moja, na hata washambuliaji wenzangu naamini wanaweza kufunga magoli katika mchezo huo, nasema hivi kwa sababu niseme niko sawa kwa kila kitu, pia timu imesajili wachezaji wenye kuleta hamasa zaidi ya kimchezo sambamba na kuengezeka kwa mwalimu Saidi Kwimbi katika benchi letu la ufundi ni dhahiri hakuna wa kunizuia nisifunge” Alisema Rais.

Katika hatua nyengine Rais amewatoa hofu washabiki wa Jang’ombe Boys juu ya mchezo huo kwa kusema kwamba, anafahamu kwamba mchezo wa mpira ni mchezo wa ushindani, lakini amewaomba washabiki wasiwe na shaka.

“Nitoe wito kwa washabiki waje kwa wingi sana kiwanjani, ili kuangalia timu yao na kuniangalia mimi jinsi nitakavotupia magoli langoni kwa KMKM na kuwafanya waogelee nyasi za uwanja wa Amani kwa huzuni na machungu nitakayowapa hio kesho, hivyo nawaomba washabiki waache wasiwasi waje kwa furaha, kwa kuwa nipo vizuri na timu kiujumla wake imeimarika Zaidi” alimalizia Rais.

Rais aliyasema hayo baada ya mazoezi ya mwisho katika kiwanja cha mazoezi kabla ya mchezo huo wa kesho wakati alipohojiwa na mwandishi wa mtandao huu.


TUNAIOMBEA TIMU YETU USHINDI MNONO.

Maoni