‘SANGULA’ ASEMA KIKOSI KIKO TAYARI KUWAZAMISHA MABAHARIA WEUSI (BLACK SAILORS FC)


Nahodha wa timu ya Jang’ombe Boys FC Ibrahim Mohammed (Sangula) amesema timu yake iko vizuri na hawana wasiwasi juu ya mchezo wao wa kesho wa ligi kuu ya Zanzibar dhidi ya Mabaharia weusi (Black Sailors), Sangula ambae ni beki kisiki wa timu hio aliyasema hayo jioni ya leo baada ya kufunga mazoezi kwa ajili ya mchezo huo.

Akizungumza na mtandao huu Sangula amewatoa khofu washabiki na wadau wa Jang’ombe Boys na kuwaahidi kwa niaba ya kikosi kitakachopngwa kesho, kwamba washabiki wasubirie kuupokea ushindi mnono.


Ibrahim Mohammed 'Sangula'

“Tumefanya mazoezi kwa muda wa wiki mbili, mazoezi yalikuwa mazuri wachezaji tumehudhuria mazoezi vizuri, tumejituma kwa pamoja, morali ya wachezaji wote imepanda kwa kiwango kikubwa na kizuri na sasa tuko tayari kuwazamisha mabaharia weusi (Black Sailor).

“Washabiki waondoe hofu kabisa juu ya matokeo ya mchezo huu, kwani kwa niaba ya wachezaji wenzangu nikiwa kama nahodha wa timu hii, sioni sababu ya kushindwa katika mchezo huu kinyume chake tutajitahidi na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu tunarudi tukiwa na pointi tatu.

“Mashabiki waje kwa wingi sana kiwanjani kwa sababu ujio wao ni muhimu sana, kwani sisi wachezaji tunaposikia sauti zao na kuona zile bendera za timu yetu sambamba na vipeperushi vyengine, huwa morali yetu inaengezeka na kuwa na hamu ya kufanya vizuri ili kuwaridhisha wao washabiki, ka sababu raha ya mpira ni washabiki na unapofanya vizuri ndio washabiki huengezeka, alisema Sangula.

Kuhusu kutokuepo Mshambuliaji machachari katika mazoezi ya leo, Sangula amesema kwamba leo mchezaji huyo amedharurika kutokana na masuala ya kifamilia, lakini usiku huu anatazamiwa kuingia kambini ili kujumuika na wenzake kwa mchezo huo.

“Kuhusu kutokuepo Khamis Mussa (Rais) leo  hapa mazoezini, kam kepteni natambua dharura yake ya kifamilia, lakini tutakuwa nae usiku huu kambini, kwa sababu ni mzima wa afya na amehudhuria mazoezi wiki zote hivyo kukosa siku ya leo tena kwa dharura za kibinadamu hakuna tatizo, alimalizia Sangula.


Baada ya mazoezi hayo timu hiyo imeondoka kuelekea kambini ambapo kesho saa 10.00 alaasiri itamenyana na Black Sailors FC, huo utakuwa mchezo wake wa pili wa ligi kuu ya Zanzibar ambapo katika mchezo wa awali Jang’ombe Boys ilitoka sare ya goli 1-1 na timu ya KMKM, goli la Jang’ombe Boys ilifungwa na Khamis Mussa (Rais).

Tunaiombea ushindi mnono timu yetu hapo kesho.

Maoni