KINACHONIPA IMANI JANG'OMBE BOYS KUIFUNGA CHARAWE LEO


Kabla ya siku ya leo timu yetu imekuwa na wiki nzuri, wachezaji wamehudhuria vizuri mazoezini, wadau na washabiki  pia na wao walijitokeza kwa wingi kuipa hamasa na sapota ya nguvu timu yao kila siku ya mazoezi, sambamba na kuonyesha mapenzi makubwa kwa wachezaji wao.

Kama hio haitoshi washabiki na wapenzi na viongozi na wao wamekuwa pamoja kujadili, kuzungumza na kupanga kwa wiki nzima juu ya mchezo huu ambao umekuwa ukisubiriwa kwa hamu na washabiki wa mpira wa miguu, ili kuona kwamba jee Charawe wataweza kuzima moto ambao umewashwa na Jang'ombe Boys, moto ambao umetoa kitisho kwa timu zilizo nafasi ya juu katika msimamo wa ligi kuu ya Zanzibar (ZPL) inayoendelea.



Charawe ambayo naweza kusema tayari imekata tiketi ya kushuka daraja, imekuwa na kawaida hio ya kuwasimamisha vigogo wa ligi kuu pindi wakikutana, ingawa mpira una matokeo matatu yaani kufungwa, kushinda na kutoka suluhu, lakini kwa uimara wa wachezaji na aina ya mazoezi sidhani kama Charawe wanaweza kutuzuia tusipate matokeo muhimu joini ya leo.

Nini kinanipa matumaini ya kwamba timu yetu itashinda katika mchezo wa leo?

UMOJA NA MSHIKAMANO WA TIMU.

Taasisi zote ulimwenguni, ili zifikie mafanikio ya malengo ni lazima angalau taasisi hio nusu na robo ya wanaounda taasisi hio, lazima wawe wamoja na washikamane.

Kwa mnasaba huo hapo tumefanikiwa kwa sababu katika timu yetu hatuna mgawanyiko wa aina yeyote, viongozi, wachezaji, wanachama, washabiki na wadau wote wapo kitu kimoja kwa lengo moja tu, nalo ni kuhakikisha mechi inakwenda vizuri na mafanikio, kitu ambacho kinanipa moya na imani kubwa ya ushindi.

MATAYARISHO MAZURI YA MCHEZO.

Tulikuwa na muda mrefu wa kujiandaa na mchezo huu baada ya kumaliza mchezo uliopita kwa mafanikio pale tulipoifunga Kilimani City 3-1, hivyo wadau wote kwa uwezo wao wametimiza wajibu wao kwa timu yao ili kujiandaa na mchezo huu ili kuupata ushindi wa timu yao.

UZIMA WA WACHEZAJI.

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwaponya wachezaji wetu wale waliokuwa wanaumwa, kwa sasa kikosi kimeimarika, Hassan Seif 'Banda' amerudi kutoka kuuguza bega lake, hivyo niseme kurudi kwa Banda kutaengeza chachu ya ushindi kwani kumekuwa na ushindani wa hali ya juu katika mazoezi kwa washambuliaji wetu watatu, nakusudia Banda, Muhamadi na Rais.

AINA YA MAZOEZI.

Hii ndio faida ya kuwa na mchezaji mwenye uzoefu wa muda mrefu na aliyepitia vilabu vingi kwa sababu ukisajili mchezaji kama huyo, huwa umesajili kocha mchezaji, maana huwa wana vitu vya ziada, kinachotakiwa ni utayari tu wa wachezaji na timu yenyewe.

Kwa sasa nampongeza sana mchezaji wetu mkongwe Abdi Kassim 'Babi', kiukweli anachokifanya sasa ndipo mahali pake hasa, kwa mfumo wa mazoezi anayoyaongoza Abdi kwa washambuliaji na viungo wetu, hakika hakuna timu itayoweza kuzuwia moto wetu.

Ukiangalia moto tuliwasha katika michezo iliyopita, kosa letu kubwa lilikuwa ni kutengeneza nafasi tumemiliki mpira mechi zote zilizopita lakini tumetengeneza nafasi chache na tatizo jengine ni kutia magoli, uwezo wetu umekuwa si zaidi ya magoli mawili licha ya kumiliki mpira kwa kiwango kikubwa, lakini kwa mfumo huu ambao 'Babi' kwa kushirikiana na Kocha Amasha, nadhani hakuna wa kutusimamisha kuanzia sasa tukianza na mchezo wa leo.

HITIMISHO.

Kwa mnasaba huo basi sina shaka na mchezo wa leo kwamba utakuwa ni wenye kutubeba, na hautatubeba bure bure bali ni kutokana na juhudi zetu, kuanzia wachezaji kwa kuhudhuria mazoezi kama kawaida na kuwa wazima wa afya, wadau na washabiki kwa jitihada zao za kihali na kimali, nasaha na mawazo yao chanya kwa viongozi wao, viongozi kwa kuwa wamoja na wasikivu kwa wanayoshauriwa, walimu kwa kuwanasihi, kuwafunza sambamba na kuwasahihisha wachezaji makosa yao pamoja na dua njema kutoka kwetu na walio upande wetu.

Muhimu zaidi tufike mapema na kwa wingi sana ili tuishangirie timu yetu kwa umoja wetu na kwa nyoyo zetu.

Jang'ombe Boys ni yetu sote.

Mungu Ibariki Jang'ombe Boys FC - AMIIN.


Maoni